Walimu watakiwa kutumia taaluma zao kuleta mapinduzi ya kimaendeleo

0

NAIBU Waziri Ofisi ya Rais – TAMISEMI Zainab Katimba amewataka walimu wote nchini kuhakikisha wanatumia taaluma na weledi wao katika kufundisha na kuleta mapinduzi ya kimaendeleo na fikra kwa jamii ya watanzania.

Katimba ametoa maelekezo hayo Juni 5, 2025 Jijini Arusha kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Mohamed Chengerwa wakati akizindua zoezi la ugawaji wa vifaa vya TEHAMA katika shule za Sekondari nchini kupitia Programu ya Kuboresha Elimu ya Sekondari (SEQUIP).

“Niwaase walimu muendelee kufanya kazi kwa bidii, kuendana na mabadiliko ya Kisera yanayoendelea kufanyika katika siku za karibuni ikiwemo kutekeleza vema mtaala ulioboreshwa, ni muhimu kujituma na kuhakikisha tafsiri ya mitaala na sera ya elimu inafanyika kwa vitendo.” alisema Katimba.

Katika kusisitiza hilo Katimba alisema, jamii ya kitanzania inamtazama mwalimu katika hatua zote za mabadiliko ya mwanafunzi hasa katika ulimwengu wa TEHAMA ambao kwa sasa unashika kasi ulimwenguni.

Aidha, ameongeza kuwa Ofisi ya Rais – TAMISEMI itaendelea kushirikiana na Wizara za kisekta na Wizara Mtambuka ili haki na maslahi ya walimu yapatikane, kulindwa na kuhakikisha wanafanya kazi katika mazingira tulivu yaliyoboreshwa na kupata huduma kwa upendo.

Kwa upande wake Joseph Mkude, Mkuu wa wilaya ya Arusha akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha alisema matumizi ya TEHAMA kwa wanafunzi yatakwenda kuongeza uelewa na ufaulu kwa wanafunzi.

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Elimu Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Dkt. Selemani Shindika alisema, vifaa hivyo vinavyogawiwa vinagarimu kiasi cha Shilingi Bilioni 12 na vitagawiwa kwa shule 422 za Sekondari ili kuimarisha ujifunzaji na ufundishaji kwa njia ya kisasa kwa kutumia TEHAMA ili kuendana na mabadiliko ya Sayansi na Teknolojia Duniani.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here