RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Hussein Ali Mwinyi amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa mstari wa mbele kuhakikisha wanawake wanapata fursa Sawa za kiuchumi kupitia Sera na Mipango mbalimbali ya Uwezeshaji.
Rais Dkt. Mwinyi alisema hayo alipozungumza katika Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliofanyika Viwanja vya Maonesho Dimani, Mkoa wa Mjini Magharibi Machi 6,2025.
Aidha, Rais Dkt.Mwinyi amewahimiza Wanawake kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi za Uongozi Muda utakapowadia.
Rais Dkt.Mwinyi amefahamisha kuwa kupitia Wakala wa Uwezeshaji Wananchi kiuchumi ZEEA wanufaika 34,746 wamefikiwa Kati yao 17,811 ni Wanawake waliochangia Asilimia 51.2 ya Wanufaika wote.
Halikadhalika Rais Dkt.Mwinyi amebainisha kuwa Serikali kupitia Wakala wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi imewezesha Utoaji wa Mikopo yenye thamani ya Shilingi Bilionii 34.9 ambapo Shilingi Bilioni 21 Sawa na Asilimia 60 zimeelekezwa kwa Wanawake.
Kwa upande mwingine, Rais Dkt Mwinyi ametoa agizo kwa Afisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Wizara inayoratibu masuala ya Majukwaa kushirikiana na Afisi ya Rais,Kazi, Uchumi na Uwekezaji, Afisi ya Rais,Tawala za Mikoa Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ, Wizara ya Biashara na Maendeleo ya Viwanda na Wadau wote Kuandaa Utaratibu wa kuhuwisha Majukwaa ya Uwezeshaji wa Wanawake Kiuchumi ili yalete matokeo yaliotarajiwa.
Vilevile, Rais Dkt.Mwinyi alizindua Mpango wa Kitaifa wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto wa 2025-2030 pamoja na Muongozo wa Uanzishwaji wa Majukwaa na Uendeshaji wa Majukwaa ya Wanawake.