Sio fikra tu zinazoweza kuenezwa, bali hata tabia mbaya

0

Na Prof. Dkt. Kudret Bulbul

KATIKA zama tunazoishi mitandao ya kijamii imechukua nafasi kubwa. Kuna mabishano juu ya faida zinazopatikana kwa muda mwingi unaotumiwa na watu katika mitandao hiyo ya kijamii kila siku.

Mitandao ya kijamii kwa baadhi ya watu imekuwa mazingira chanya ya kujumuika, lakini kwa watu wengine imekuwa katika hali hasi ya kuwapelekea kujitenga. Kila kitu kipo kwa uhuru na furaha, lakini ni mazingira ambayo yanabidi kufanyiwa mabadiliko.

Ni kivipi tuitathimini mitandao ya kijamii? Cha kwanza tunachoweza kusema ni kwamba, tuitathimi au tusiitathimi mitandao ya kijamii ipo katika maendeleo ya kiaina yake ikiendelea kuchukua sura mpya siku hadi siku, lakini hilo haliwezi kutuzuia sisi kuifanyia tathimini mitandao hiyo.

Ni mazingira yanayotoa kila aina ya fikra, uhuru na fursa za bure. Tukianza kwa kuziangalia faida za mitandao ya kijamii, Mitandao ya kijamii hutoa fursa isiyo na kifani kwa wale wenye fikra ambao wanataka fikra zao ziwafikie watu wengine, na kwa wale wenye mshawasha wa kutaka kujua watu wengine wanafikiria nini.

Imekuwa ni kitu kinachowezekana kupata fikra za watu Kitaifa na Kimataifa ambazo katika hali halisi ilikuwa ni vigumu kuzipata. Ukiangalia kwa mtazamo mwingine kupitia mitandao ya kijamii unaweza kufahamu ni fikra gani wanazo watu walio mbali na wewe kiuhalisia.

Kikubwa zaidi ni kwamba, haihitaji kutumia gharama kubwa kubadilishana fikra. Hapo zamani ilihitajika gharama kubwa kutoa gazeti kwa ngazi ya Kitaifa, ilihitajika gharama kubwa mno kuanzisha kituo cha redio au luninga. Mitandao ya kijamii imewezesha kila mtu aweze kubadilishana fikra tena kwa mapana na kwa gharama ndogo.

Kwa upande mwingine kubadilisha fikra bila kuwapo kwa mipaka, kila mtu aseme tu anachofikiria inaweza kuwa kitu hatari kwa mamlaka hasa kwa jamii zilizojifungia mfano.

Tawala za kiarabu zilizoweza kudumu kwa maelfu ya miaka wakiwa wamejifungia zilianza kubadilika baada ya vuguvugu la uamsho la Uarabuni, ambapo tunaweza kuona moja ya sababu kubwa ilikuwa ni mitandao ya kijamii kwa sababu kupitia mitandao hiyo ni rahisi kukusanya watu kwa wingi na kufanya upinzani.

Ni mazingira ambayo uongo wa aina yeyote unaweza kusambazwa, na watu wanaweza kurubuniwa. Kwa upande mwingine mitandao ya kijamii ni mazingira ambayo uongo wa kila aina unaweza kusambazwa. Katika mitandao ya kijamii ni vigumu kubaini kipi ni ukweli na kipi ni uongo.

Katika mitandao ya kijamii sio tu fikra zinazoweza kuenezwa bali hata tabia mbaya, utovu wa sheria, na uhalifu huweza kuenezwa kupitia mitandao hiyo. Muanzilishi wa mtandao wa Facebook, Zuckerberg, katika kujilinda dhidi ya wahalifu wa kimtandao ameziba kamera na kipaza sauti cha ‘laptopu yake kwa tepu.’

Kwa watu wenye nia ovu ni rahisi kurubuni kundi la watu kuwa kutumia mitandao ya kijamii, fursa hii huweza kutumiwa ipasavyo na mashirika ya kijasusi.

Tuliona jinsi watu walivyo hamasiswa na kuzua balaa katika maandamano ya Taksim kisa kukatwa kwa miti michache katika bustani za Gezi. Tumeona katika Mataifa mengine maandamano vizibao vya njano, rangi ya chungwa hata harakati za mapinduzi ya Kadife.

Unapozungumzia madhara ya kijamii huwezi kuacha kuzungumzia ulaghai na propaganda. Ajenda za kina na za siri huweza kuendeshwa kwa kutumia anwani za uongo ili kufikia lengo fulani, au kuhujumu watu, chama au shirika fulani wanaoonekana kupinga ajenda.

Kupitia propaganda baadhi ya ukweli hufichwa na picha iliyojengwa ndio hufanywa kuwa ukweli. Kwa wapangaji wa njama wenye nia ovu wao hutumia mitandao ya kijamii kama chombo cha mashambulizi.

Tunapofanya tathimini juu ya mitandao ya kijamii tunapaswa kufahamu kwamba, mashirika haya yana taarifa zetu nyingi. Taarifa hizi ni zaidi ya taarifa zetu binafsi tunazozitawanya, kupitia maoni unayotoa, au unachokipenda katika mitandao ya kijamii, mashirika haya yana taarifa za kutosha juu ya mtu binafsi, jamii kiasi cha kuweza kufanya upembuzi juu ya utambulisho, dini, kabila na kila aina ya utambulisho.

Mfano kwa kuzingatia unachokipenda katika mitandao ya kijamii tathimini hufanywa na wewe kuletewa mapendekezo juu kitu cha kufanya kwa marafiki zako, kwa mwelekeo huo huo taarifa nyingi ambazo mashirika haya ya mitandao ya kijamii yanazimiliki zinayawezesha kuitazama dunia kwa jicho la runinga na kuitathimini kama vile mwandishi George Orwell anavyozungumzia katika riwaya yake ya mwaka 1984 “tele-screen”.

Mashirika ya kijasusi yanayofanya kazi na mashirika ya mitandao ya kijamii huwezesha serikali zao kuwa na nguvu isiyomithilika. Hata hivyo mashirika hayo ya mitandao ya kijamii hayatoi taarifa hizo bure kwa mashirika ya kijasusi.

Fikiria taarifa tunazoyapa mashirika haya maoni yetu katika kila tukio, tupo maeneo gani, tunafanya nini, tunakabiliana na matukio gani, tunachukua upande gani n.k, taarifa zote hizo kutuhusu mashirika hayo yanazo. Maoni, kupenda na machapisho tunayoyachapisha katika mitandao ya kijamii, kila siku yamekuwa yakifanyiwa tafiti na kulinganishwa na mamilioni ya mada za kitafiti kuhusiana na maoni ya jamii.

Matokeo ya tafiti hizi hutumiwa na mashirika hayo kufanya tathimini za muda mrefu na hivyo basi kuyafanya mashirika haya kuwa na taarifa ambazo hata Mataifa, mashirika, jamii na watu husika hawana.

Mashirika haya hayafanyi tu tathimini za aina moja, hutafiti kuanzia aina ya utu “personality” ya mtu, dini, utamaduni, jamii, siasa na mambo mengine yanayopendelewa kama aina ya matumizi unayoweza kufanya, mtazamo wa dunia ya nje, unachoepuka n.k. Hali hii inapaswa ifahamike na kila nchi kwa mustakabali wa nchi hiyo.

Kwa watu wenye umri fulani kama wangu inawezekana wanaitathimini mitandao ya kijamii kwa namna fulani au hawaitathimini. Lakini, kwa upande wa umri fulani kushuka chini wao wamezaliwa na wanakuwa ndani ya mitandao ya kijamii.

Katika mazingira ambayo watoto hukua, kwa sababu ya kupungua kwa uhusiano wa kifamilia, elimu na mazingira halisi ya kijamii yanazidi kupoteza maana, mitandao ya kijamii inazidi kuwa mahali pekee pa kujumuika kwa watoto wetu.

Je, ni wapi watoto wetu watapelekwa na mazingira ambayo hakuna sheria, kanuni, fadhila lakini “trawl” ajenda za siri na kupotosha, viko kwa sehemu kubwa miongoni mwa watumiaji? Je, Mazingira haya yanaunda ulimwengu gani?

Sijakata tamaa kabisa. Kama nilivyosema, licha ya madhara na uharibifu wake, mitandao ya kijamii inatoa fursa nzuri. Kwa kufahamu mazingira ya mitandao ya kijamii inawezekana pia kuitathimini kwa mtazamo wa chanya.

Kwa upande wa watoto wetu, tunachohitaji kufanya sio kuwaachisha kutumia mitandao ya kijamii, lakini tuwafanye waachane na njia hizo baada ya kushirikiana kwa kiwango fulani kwa kutekeleza majukumu yetu.

Kwa kifupi kama ilivyo mchakato wa utandawazi, mitandao ya kijamii nayo inazidi kusonga katika mkondo wake bila kujali tathimini tunayoifanya kuihusu. Tunachohitajika kufanya sio kupinga au kuunga mkono, bali ni kuhakikisha mkondo wa mitandao ya kijamii unakuwa na faida kubwa zaidi na hasara ndogo zaidi kwetu, kwa familia zetu, nchi zetu na kwa binadamu wote kwa ujumla.

*Mwandishi wa Makala hii ni Mkuu wa kitivo cha siasa Chuo Kikuu cha Ankara.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here