Mradi wa TACTIC kuboresha mazingira ya biashara Singida

0

NAIBU Waziri wa Ofisi ya Rais – TAMISEMI Zainab Katimba amesema kukamilika kwa utekelezaji wa miradi ya uboreshaji miundombinu ya Miji Tanzania (TACTIC) awamu ya pili katika Manispaa ya Singida kutaleta mabadiliko chanya kwenye huduma, manunuzi na mazingira bora ya kufanyia biashara kwa wajasiriamali na wafanyabiashara wa Mkoa wa Singida.

Katimba amebainisha mkoani Singida katika Manispaa ya Singida mara baada ya kushuhudia utiaji saini Mkataba wa ujenzi wa soko la Kimataifa la Vitunguu, ujenzi wa barabara za katikati ya mji na viwandani kilomita 7.52, ujenzi wa mtaro wa maji ya mvua wa kilomita 2.6 pamoja na Ofisi ya uratibu.

Akizungumzia Ujenzi wa soko la vitunguu, Katimba amebainisha kwamba jengo litakalojengwa litakuwa la ghorofa mbili, likiwa na maeneo maalum ya kuchambua na kukaushia vitunguu, maduka na vyumba vya huduma za kifedha.

Aidha, jengo hilo litakuwa na uwezo wa kuhudumia wafanyabiashara 3000 kwa wakati mmoja, makadirio yakiwa ni kuingiza mapato ya Shilingi Milioni 505 kwa mwaka tofauti na Milioni 300 za sasa zinazotokana na wafanyabiashara 1069 wanaoweza kuhudumiwa na soko la sasa.

Aidha, katika maelezo yake kando ya kupongeza waratibu wa mradi huo kwa kutoa nafasi kwa mkandarasi mzawa, Katimba amemuagiza Mkandarasi M/s Sihotech Engeneering Company Limited kukamilisha mradi huo kwa wakati, ili tija ionekane mapema kwa wananchi wanaotarajiwa kuwa wanufaika wa mradi huo.

Amewasihi pia wananchi wa Manispaa ya Singida kutoa ushirikiano kwa Mkandarasi anayetekeleza mradi huo, pamoja na kutunza miundombinu hiyo pale itakapokamilika ili iweze kuwa na tija iliyokusudiwa kwa muda mrefu zaidi.

Katimba ameziagiza Halmashauri zote nchini zenye miradi ya TACTIC kusimamia vyema uendeshaji wa masoko na vituo vya mabasi ili kuzalisha mapato yaliyotarajiwa na Serikali kwa maendeleo ya maeneo yao.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here