Na Hilary Shuma – OR-TAMISEMI
KAIMU Katibu Tawala wa Mkoa wa Lindi, Nathalis Linuma, amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeendelea kutoa mafunzo kwa Maafisa Tarafa na Watendaji wa Kata wapya kwa lengo la kuwawezesha kutoa huduma bora kwa wananchi kwa weledi na ufanisi.
Linuma ameyasema hayo katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Lindi wakati akifungua rasmi mafunzo elekezi kwa Maafisa Tarafa na Watendaji wa Kata walioajiriwa hivi karibuni.
Alisema, mafunzo hayo ni muhimu katika kuwajengea uwezo wa kiutendaji, kuelewa majukumu yao kikamilifu na kuongeza ufanisi katika kuwahudumia wananchi.
“Mafunzo haya yameandaliwa ili kuwasaidia Watendaji wapya kukabiliana na changamoto mbalimbali za kiutendaji, kama vile utatuzi wa migogoro ya kiutawala, usimamizi hafifu wa miradi ya maendeleo na uelewa mdogo wa sera na miongozo ya Serikali,” alisema Linuma.
Ameongeza kuwa, kupitia mafunzo haya, washiriki wataweza kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato, usimamizi wa rasilimali za umma kwa uadilifu, kushughulikia changamoto za wananchi kwa ukaribu zaidi na kuimarisha mawasiliano kati ya Serikali na wananchi.
Mafunzo hayo yameandaliwa na Ofisi ya Rais – TAMISEMI kwa kushirikiana na Chuo cha Serikali za Mitaa (LGTI) na Chuo cha Utumishi wa Umma (TPSC), ambapo mada mbalimbali zitawasilishwa zikiwemo: Maadili ya Utumishi wa Umma, Usimamizi wa Miradi ya Maendeleo, Ufuatiliaji wa Mipango ya Serikali, Sheria na Kanuni za Utendaji Kazini, pamoja na mbinu za kushughulikia kero na malalamiko ya wananchi kwa wakati.
Linuma amesisitiza kuwa, mafunzo haya pia ni utekelezaji wa Waraka wa Utumishi Na. 5 wa Mwaka 2011 unaoelekeza utoaji wa mafunzo elekezi kwa Watumishi wa Umma.
Tangu mwaka wa fedha 2022/23, zaidi ya Maafisa Tarafa 538 na Watendaji wa Kata 3,900 wameshapatiwa mafunzo hayo