OR – TAMISEMI
NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko, ameitaka jamii kuthamini nafasi ya familia katika makuzi na malezi ya mtoto, kama hatua ya msingi katika kudhibiti vitendo vya watoto kukimbia familia zao na kuwa watoto wa mitaani.
Naibu Waziri Mkuu Dkt. Biteko ametoa agizo hilo leo Mei 24, 2025, katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Familia na kilele cha Kongamano la Malezi lililofanyika jijini Mwanza.
Ameeleza kuwa, ni muhimu kuzingatia malezi bora ya mtoto tangu akiwa tumboni kwa mama hadi anapofikia umri wa miaka 18, na serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imekuwa ikitekeleza Programu Jumuishi za Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto kwa kipindi cha 2021 hadi 2026.
Dkt. Biteko amezindua Mwongozo wa taifa wa uanzishaji na uendeshaji wa vikundi vya wazazi vya malezi na matunzo ya mtoto, na mwongozo wa Watoto kwa muktadha wa dini ya Kikristo na Kiislamu pamoja na kuzindua kampeni maalum ya malezi kwa Watoto.