RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali inaendelea kutafuta vyanzo vipya na nafuu vya fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati na kuharakisha maendeleo ya Zanzibar.
Rais Dkt. Mwinyi amesema hayo leo, tarehe 10 Agosti 2026, alipokutana na Rais na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Trade and Development Bank (TDB), Admassu Tadesse, pamoja na ujumbe wake Ikulu Zanzibar.
Amesema Zanzibar inalenga kutumia mifumo mbalimbali ya kifedha ili kuongeza fursa za uwekezaji katika miradi muhimu ikiwemo Bandari Jumuishi ya Mangapwani, nishati, makaazi, mafuta na gesi, pamoja na miradi ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza umuhimu wa ushirikiano na taasisi za fedha za kimataifa na sekta binafsi katika kupata mitaji yenye masharti nafuu na kuimarisha utekelezaji wa vipaumbele vya maendeleo ya Zanzibar.
Kwa upande wake, Admassu Tadesse ameihakikishia Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ushirikiano wa karibu wa TDB katika kuwezesha miradi yenye tija kupitia mifumo mbalimbali ya kifedha, ikiwemo fedha za maandalizi ya miradi, uwekezaji na mitaji nafuu.