Rais Samia achangia Milioni 50 Ujenzi wa Madarasa

0
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni akimkabidhi zawadi mshindi wa kwanza wa mashindano ya kusoma Qur'ani Ismail Khalid (kushoto), yaliyofanyika wakati wa Hafla ya Kumbukumbu ya Kusheherekea kuanzishwa kwa Taasisi ya Maawal Islamiy na kumbukumbu ya Muanzilishi, Sheikh Shabaani Mohamed Hariri. Hafla hiyo imefanyika jijini Tanga ambapo Waziri Masauni alialikwa kuwa mgeni rasmi. Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Na Mwandishi Wetu, Tanga

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan amechangia kiasi cha Shilingi Milioni 50 katika Ujenzi wa Majengo ya Taasisi ya Elimu ya Maawal Islamiya iliyopo jijini Tanga ikiwa ni muendelezo wa Serikali wa Awamu ya Sita kuunga mkono jitihada za wadau katika kutoa elimu.

Kiasi hicho cha fedha kimewasilishwa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni wakati akihutubia mamia ya waumini wa kiislamu waliokusanyika kusheherekea kuanzishwa kwa taasisi hiyo na kumbukumbu ya Muanzilishi,Sheikh Shabaani Mohamed Hariri ambapo pia alifikisha salamu kwa waumini hao kutoka kwa Rais Samia huku akigusia kuwepo kwa mporomoko wa maadili unaosababisha uhalifu katika sehemu mbalimbali za nchi.

Waumini waliokusanyika wakati waHafla ya Kumbukumbu ya Kusheherekea kuanzishwa kwa Taasisi ya Maawal Islamiy na kumbukumbu ya Muanzilishi, Sheikh Shabaani Mohamed Hariri wakiomba dua ya pamoja kumuombea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan baada ya kupokea mchango wa Shilingi Milioni 50 kwa ajili ya kuchangia ujenzi wa madarasa yanayojengwa katika taasisi hiyo.Hafla hiyo imefanyika jijini Tanga ambapo Waziri Masauni alialikwa kuwa mgeni rasmi.Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

“Naomba nitumie fursa hii kuwasilisha salamu za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati nakuja nilimuaga amesema niwasalimie sana na ametoa kiasi cha Shilingi Milioni Hamsini ikiwa ni mchango wake katika ujenzi wenu wa majengo ya madarasa unaoendelea hapa”

“Niwaombe pia mumuombee dua ili aweze kuiongoza nchi yetu kwa salama na amani, lakini kumekuwepo na mmomonyoko wa maadili niwaombe viongozi wa dini muendelee kutumia sehemu zenu za ibada kuiasa jamii iachane na mila na tamaduni ambazo zipo kinyume na mafundisho ya dini zetu” alisema Waziri Masauni.

Wakizungumza wakati wa hafla hiyo, Sheikh wa Mkoa wa Dodoma, Mustafa Rajab Shabaani na Sheikh wa Mkoa wa Pwani, Alhaji Khamis Mtupa walisisitiza kulindwa kwa maadili katika jamii ambayo yameendelea kuporomoka katika jamii huku wakiwataka waumini kuendelea kuwa karibu na watoto ili kufahamu changamoto mbalimbali wanazokutana nazo.

Sheikh wa Mkoa wa Pwani, Alhaji Khamis Mtupa akizungumza wakati wa Hafla ya Kumbukumbu ya Kusheherekea kuanzishwa kwa Taasisi ya Maawal Islamiy na kumbukumbu ya Muanzilishi, Sheikh Shabaani Mohamed Hariri. Hafla hiyo imefanyika jijini Tanga ambapo Waziri Masauni alialikwa kuwa mgeni rasmi.Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

“Jamii imekumbwa na mabalaa mbalimbali watu wamekua na unyama usiomithilika mpaka imefikia sasa hivi wazazi kuambiwa kuwakagua watoto katika maumbile yao kila wanapotoka shuleni sasa tuitake jamii iwe karibu na watoto ili kuweza kubaini changamoto zao mbalimbali wanazokutana nazo kwani kutokua nao karibu upelekea watoto hao kukumbana na mabalaa lakini kutokuwepo ukaribu kati ya mzazi na mtoto upelekea mtoto kukaa kimya wakati tayari ashaathirika.” alisema Sheikh Mtupa.

Taasisi hiyo ya Maawal Islamiy ina miaka 44 tangu ianzishwe na Sheikh Shabaan Hariri ikijikita zaidi katika kutoa elimu,misaada kwa watu mbalimbali wenye uhitaji na huduma za afya.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here