Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
CHAMA cha Mapinduzi (CCM) kimesema mtanzania yeyote ambaye hataona kazi kubwa ya kimaendeleo iliofanywa na Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, haraka aende kituo chochote cha Afya akapime uoni wa macho yake.
Pia, chama hicho kimejigamba kuwa maendeleo ya haraka yaliyopatikana katika Awamu ya Sita, yamezishangaza nchi nyingi jirani na kuupongeza utawala wa Rais Samia.
Matamshi hayo yametamkwa na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar, Idara ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Khamis Mbeto Khamis aliyesema Rais Samia amefanya maajabu katika uongozi wake kwa kusimamia sera za maendeleo.
Mbeto alisema, kazi ya usimamiaji na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kihuduma na kimaendeleo imetekelezwa kwa ufanisi na Serikali, hivyo haihitaji kuona kwa tochi, badala yake yaliyofanyika yanaonekana.
Alisema, Rais Dkt. Samia ni kati ya marais ambao wametimiza vyema majukumu na wajibu wao mbele ya wananchi kwa kuendeleza na kuanzisha miradi ya kupigiwa mfano ambayo imeacha alama zisizofutika.
“Tanzania ya leo itabaki kuwa mfano mbele ya Mataifa mengine Barani Afrika. Serikali ya Awamu ya Sita imefanya maajabu makubwa sana. Mikoa yote imepata mabadiliko kiuchumi huku wananchi wakiishi maisha bora,” alisema Mbeto.
Akitoa mfano, Katibu huyo Mwenezi aliitaja sekta ya afya chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Tanzania imetambulika na Asasi za Kimataifa na kupokea Tuzo Maalum ya Kimataifa ya Global Goalkeeper Award kutoka Taasisi ya Gates Foundation.
Aidha, Tuzo hiyo inaashiria kutambua mchango na jitihada zilizofanywa kwenye sekta ya afya na mafanikio ya Serikali ya Tanzania katika kupunguza vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga chini ya umri wa miaka mitano.
Alisema, Tuzo hiyo ambayo hutolewa kwa viongozi waliowezesha nchi zao kuharakisha maendeleo kuelekea kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu (Sustainable Development Goals –SDG’s) imekabidhiwa kwa Rais Dkt. Samia na Dkt. Anita Zaidi, Rais wa Kitengo cha Usawa wa Jinsia kutoka Taasisi ya Gates.
“Kati ya mwaka 2020 hadi 2024 uwekezaji uliofanywa na Serikali kwenye sekta ya afya imewezesha Tanzania kuongeza vituo vya kutolea huduma za afya vinavyotoa huduma za dharura za mama na mtoto kutoka 340 hadi 523,” alieleza Mbeto.
Pia, Wataalamu wabobezi wa kiafya wa masuala ya mama na mtoto wameongezeka kutoka 69 hadi 338, na kuongeza mashine za Ultrasound na Somograph kutoka 345 hadi 970.
Mbeto alisema, mwaka 2020 Hadi 2024 Serikali ya Rais Dkt. Samia iliongeongeza Vituo vya Afya Maalum kwa Mama na Mtoto.