Maagizo ya Dkt. Mpango kwa Waziri wa Fedha

0
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Isdor Mpango, akimsikiliza mmoja wa wadhamini (hayupo pichani) wakati wa hafla ya ufunguzi wa Kongamano la Wanawake la Nishati Safi ya kupikia iliyofanyika katika Ukumbi wa Jakaya Kikwete Convention Centre, Jijini Dodoma.

Na Josephine Majura na Asia Singano WF Dodoma

MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Isdor Mpango amemuagiza Waziri wa Fedha Dkt Mwigulu Lameck Nchemba, kuangalia uwezekano wa kupitia viwango vya kodi kwa majiko yanayotumia nishati safi ya kupikia hasa kipindi hiki ambacho maandalizi ya bajeti ijayo yanafanyika.

Maagizo hayo ameyatoa wakati akifungua Kongamano la wanawake la kugawa mitaji na vitendea kazi vya nishati safi ya kupikia, lililofanyika katika ukumbi wa Jakaya Kikwete Convention Center Jijini Dodoma.

Aidha, Mpango amezitaka Sekta Binafsi nchini kutumia fursa ya kutokomeza matumizi ya nishati chafu kama njia moja wapo ya kuongeza kipato chao na kukuza uchumi wa nchi.

‘’Natoa wito kwa sekta binafsi kuunga mkono na kuchangia katika kampeni ya kuondokana na matumizi ya nishati chafu. Baadhi ya maeneo ambayo sekta binafsi inaweza kusaidia ni kuwekeza katika utafiti, ubunifu na uzalishaji wa nishati safi na nafuu ya kupikia’’ alisema Dkt. Mpango.

Aliongeza kuwa, matumizi ya nishati chafu kama vile mkaa na kuni yameleta athari kubwa zaidi kiafya kwa wananchi hususani wanawake ikiwa ni pamoja na kupoteza maisha.

‘’Wanawake huvuta moshi mwingi wenye viwango vikubwa vya sumu, ambazo husababisha magonjwa ya mfumo wa hewa yanayosababisha vifo takriban 33,000 vya watanzania kila mwaka’’ alisisitiza Dkt. Mpango.

Kongamano hilo limefanyika kama sehemu yakuunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhamasisha wanawake kutumia nishati safi ikiwa ni wiki ya maadhimisho ya siku ya wanawake duniani.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here