Na Mwandishi Wetu, Pemba
CHAMA Cha Mapinduzi kimesema viongozi wa ACT Wazalendo bila kulitaja jina la Marehemu Maalim Seif Sharif Hamad, hawana uwezo wa kukubalika katika jamii na kupata viti vya Udiwani, Uwakilishi, Ubunge na kuongeza kura za Urais.
Kimesisitiza kuwa ndio maana hueneza na kuhubiri siasa za utengano, shari au kukimbilia kukosoa mfumo wa Muungano wa Serikali mbili si sahihi ili wapatwe kusikilizwa.
Katibu wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar, Idara ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Khamisi Mbeto Khamis, ameeleza hayo akiwa katika ziara ya kizazi huko Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba.
Akizungumza na wanachama wa CCM, Wilaya hiyo, Mbeto alisema kisiasa ACT Wazalendo kimeshakwama, hakina maneno ya kuwashawishi wananchi ili kiweze kukubalika na kuchagulika katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba Mwaka huu.
Mbeto alisema, baada ya chama hicho kukosa sera zenye matumaini kwa wananchi, kinga yao kuu ni kulitumia jina la Maalim Seif, kuhubiri siasa za fitna, majungu na ubaguzi au kuzungumzia muundo wa Muungano.
“Jusa na viongozi wenzake hawana uwezo wa kuwaeleza lolote waZanzibari wakasilizwa na kufahamika. Wana dosari na shutuma katika jamii zisizowapa heshima. Baada ya kujua wana udhaifu huo, jina la Maalim Seif kwao huwa ngao yao,” alisema Mbeto.
Alisema, iwapo kungekuwa na tija ya kuzungumzia kasoro za chaguzi zilizopita CCM kingezungumzia chaguzi za mwaka 1957, 1961 na 1963, lakini hakioni kama kuna umuhimu wowote.
Alisema, ACT kinapozungumzia chaguzi za mwaka 1995 hadi 2015 ni katika kuiaminisha jamii katika uongo wao wa kudai kuwa hakuna ambao CCM kilishinda kama kinavyojidanganya.
“Kuzungumzia uchaguzi uliopita ni kutonesha vidonda vilivyoanza kupona. CCM na ACT vyote havitakiwi kuzungumzia chaguzi zilizopita. Kufanya hivyo ni kupoteza wakati bure. Ni sawa na kufufua makaburi ya wafu,” alieleza.
Alisema, kwa vyovyote itakavyokuwa, Zanzibar haiwezi kujitoa katika Muungano wa Serikali mbili ili Mataifa ya Tanganyika na Zanzibar yawe na mamlaka kamili kama ilivyokuwa kabla ya Aprili 26 mwaka 1964.
“Serikali ya Rais Dkt. Hussein Ali Mwinyi ina cha kuwaonyesha wananchi kwa iliofanyika miaka mitano iliopita. Yaliyofanyika yanaonekana na kila mZanzibari. Rais Dkt. Mwinyi hana kazi ngumu Oktoba mwaka huu,” alisema Mbeto.
Hata hivyo, Katibu huyo Mwenezi aliwataka wananchi wa mkoa wa Kaskazini Unguja kutazama mema waliofanyiwa na serikali ya awamu ya nane Zanzibar na manufaa walioyapata.