RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ameyakaribisha makampuni na wawekezaji kutoka Uturuki kuwekeza nchini, hususan katika sekta za biashara, nishati na miundombinu.
Rais Dkt. Mwinyi ametoa wito huo alipokutana na Mkurugenzi Mkuu anayeshughulikia masuala ya Afrika kutoka Wizara ya Mambo ya Nje ya Uturuki, Balozi Volkan Isikci, aliyefika Ikulu, Zanzibar, akiongozana na Balozi wa Uturuki nchini Tanzania, Balozi Bekir Geze.
Amesema hatua hiyo itasaidia kuimarisha uhusiano wa kihistoria kati ya nchi hizo mbili na kufungua fursa mpya za ushirikiano katika biashara na uwekezaji.
Aidha, amesisitiza umuhimu wa wawekezaji kuwekeza katika sekta za kimkakati zikiwemo nishati, kilimo, utalii, afya na miundombinu, pamoja na kuongeza thamani ya mazao ya ndani.
Kwa upande wake, Balozi Isikci ameihakikishia Zanzibar kuendelea kushirikiana na kuunga mkono juhudi za maendeleo ya kiuchumi kupitia sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya, kilimo na utalii.