TPDC wachangia Milioni 100 kupitia ‘Marathon’

0

Na Mwandishi Wetu

Shilingi Milioni 100 zimetolewa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kupitia mbio za TPDC Marathon msimu wa kwanza kwa ajili ya kuchangia matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete.

Akikabidhi hundi ya fedha hizo leo katika viwanja vya Farasi vilivyopo Oyster bay jijini Dar es Salaam Rais wa Awamu ya Nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alisema, mbio za TPDC zimeanza na madhumuni mazuri ya kusaidia na kugharamaia upasuaji wa moyo kwa watoto 50 wenye matatizo ya moyo wanaotibiwa JKCI.

Kikwete alisema, upasuaji wa moyo una gharama kubwa, hivyo mtu akiwa na lengo la kugharamia matibabu kwa wale ambao hawana uwezo wa kiuchumi inapendeza ndani ya jamii yetu, kwani hii inaonyesha dhumuni la kuiunga mkono Serikali ambayo baada ya kuona jamii ina uwezo mdogo wa kiuchumi ikasukumwa kujenga Taasisi hiyo ili wananchi wake wapate huduma kirahisi.

“Hapo awali Tanzania tulilazimika kupeleka wagonjwa nje kwa matibabu ambapo gharama yake ilikua dola elfu saba kwa kila mgonjwa ambayo ni ngumu kwa mtu wa kawaida kumudu matibabu, lakini pia Serikali ilikua na mzigo mkubwa hivyo kutupa motisha ya kuanza safari ya kujenga uwezo wetu wa ndani ambao leo hii tunaona matunda yake”,

Dkt. Kikwete alisema, JKCI ndani ya miaka saba tangu kuanzishwa kwake imekua kituo cha ubingwa kinachotoa huduma za matibabu ya moyo kwa ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, hivyo kuwataka wadau kujitokeza kushirikiana na JKCI ili kufanikisha lengo lake la kuokoa maisha ya watanzania na kupunguza idadi ya watoto wanaosubiria kufanyiwa upasuaji wa moyo.

“Tusingekuwa na Taasisi hii sina hakika wale wote ambao wameshapata matibabu JKCI wangekuwa sasa hivi wako katika hali gani, kwasababu tangu kuanzishwa kwa Taasisi hii jumla ya wagonjwa wa moyo elfu saba na mia sita wameshafanyiwa upasuaji wa moyo”,

“Nawapongeza wataalam wote waliopo katika Taasisi hii kwa hatua kubwa waliyopiga na kuiheshimisha nchi yetu kwa kutoa msaada kwa watanzania wenzetu, Tunaokoa maisha ya watu wengi na hadi sasa kuna watoto 511 wanaohitaji matibabu haya wapo kwenye foleni ya kusubiri huduma ya upasuaji wa moyo”, alisema Dkt. Kikwete.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Shirika la Mafuta la Taifa (TPDC) Dkt. James Mataragio alisema, kuiachia Serikali yenyewe kufanikisha huduma za matiababu kwa watu wasiokuwa na uwezo haiwezekani inahitaji pia watu wengine ili maisha ya watoto wenye magonjwa ya moyo yaokolewe.

“Nawashukuru wakimbiaji wote kwa kujitokeza siku hii ya leo kuweza kutuunga mkono kuchangia watoto wenye magonjwa ya moyo, naamini wote mlioshiriki mmekubali na kuguswa kuchangia watoto ambao wanatuhitaji ili kufanikisha matibabu yao”,

“TPDC imekua ikijishughulisha na kufanya kazi na jamii mbalimbali ambazo zinatuzunguka kwa kuchangia katika masuala ya elimu, michezo na shughuli mbalimbali za kijamii lakini leo tumeona twende katika hatua nyingine ya kusaidia kuokoa maisha ya watoto wenye magonjwa ya moyo”, alisema Dkt. Mataragio.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi alisema, kila mwaka Tanzania wanazaliwa watoto Milioni 2 ambapo asilimia 0.8 mpaka 1 ya watoto wanaozaliwa wanakuwa na matatizo ya moyo na katika hao asilimia 25 uhitaji upasuaji wa moyo.

“Toka kuanzishwa kwa Taasisi yetu kila mwaka tumekuwa tukifanya upasuaji wa moyo kwa watoto kati ya 250 na 300, kupitia mbio za TPDC Marathon watoto 50 wamechangiwa shilingi milioni 100 ambapo kila mtoto amechangiwa milioni 2 na fedha nyingine iliyobaki katika matibabu ya watoto hao itajaziwa na Serikali”,

“Tunawashukuru sana TPDC kwa kuguswa kuchangia matibabu ya watoto wetu, kupitia msaada huu tunaweza kuwafanyia upasuaji watoto wote 50 ndani ya mwezi mmoja na kuwamaliza”, alisema Prof. Janabi.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here