TGC yajipanga kuwa kituo bora uthaminishaji madini Afrika

0

Na Samwel Mtuwa, Arusha

KITUO cha Jemolojia Tanzania (TGC) kimejipanga kuwa Kituo bora cha mafunzo ya utambuzi, uthaminishaji, ukataji madini ya vito, uchongaji wa vinyago vya vito pamoja na utengenezaji wa bidha za urembo na mapambo vya madini barani Afrika.

Hayo yamebainishwa na Kaimu Mratibu wa Kituo hicho, Jumanne Shimba wakati akizungumza na waandishi wa habari za mtandaoni wanaofanya ziara ya kutembelea Kituo hicho kilichopo mkoani Arusha.

Shimba alisema, TGC tayari Wizara ya madini kupitia TGC imesaini hati za makubaliano (MoU) na Chuo cha Jemolojia cha nchini Thailand yenye lengo la kushirikiana ya katika masuala ya uongezaji thamani madini ambapo ametabanaisha kuwa tayari wameshaanza kuandaa mpango kazi wa kutekeleza makubaliano na Gem and Jewellery Institute of Thailand (GIT).

Sambamba na hapo, Kituo kimesaini hati za makubaliano (MoU) na Wizara ya Maji, Nishati na Madini ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar yenye lengo la kushirikiana katika masuala ya uongezaji thamani madini ili ujuzi huo uweze kunufaisha watanzania wengi zaidi.

Akielezea kuhusu mpango wa wanafunzi kupata mikopo kutoka Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu, amesema mpaka sasa wanafunzi 11 wamefanikiwa kupata mikopo.

Akielezea kuhusu mikakati ya Kituo, Shimba amebainisha kuwa, kwa sasa Kituo kina mpango wa kuunganisha sekta ya uongezaji thamani madini na Sekta nyingine za kimkakati ikiwemo Sekta ya Utalii kwa lengo la kuvuka mipaka ya masoko kwa huduma zinazotolewa na bidhaa zinazotengenezwa kituoni.

Alieleza kuwa TGC inatoa mafunzo ngazi cheti hadi diploma katika teknolojia ya vito na usonara, ambapo sifa za kujiunga ngazi ya cheti ni mtu yeyote aliye na nia ya kujifunza ujuzi wa kuongezea thamani madini na ngazi ya Diploma ni mtanzania aliyehitimu kidato cha nne na kupata ufaulu katika masomo manne kuanzia daraja D.

Aidha, Kituo kinaangalia uwezekano wa kuanzisha viwanda vya kutengeneza bidhaa maeneo yanayozalisha madini ya vito na metali za thamani akitolea mfano Mkoa wa Geita, Wilaya za Kahama , Chunya, Morogoro na Mji wa Mirerani.

Kituo cha TGC kilianzishwa mwaka 2003, ikiwa ni utekelezaji wa Sera ya Madini ya Mwaka 1997, kabla ya hapo kilijulikana kwa jina la Arusha Gemstone Carving Centre (AGCC).

Kutokana na kupanuka kwa shughuli za Kituo na kuongezeka kwa manufaa yatokanayo na madini, katika kutekeleza Sera ya Madini ya Mwaka 2009, ilipofika mwaka 2010 jina lilibadilika na kutambulika kama Tanzania Gemological Centre (TGC).

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here