‘Serikali ya Umoja wa Kitaifa imeondoa siasa za chuki na uhasama’

0
Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi.

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi amesema, uamuzi wa kuwepo kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa ya Zanzibar ulizingatia kutanguliza mbele usalama wa maisha ya watu, maslahi, utulivu na mstakabali mwema wa Zanzibar, Wazanzibar na Watanzania wote kwa ujumla, kuliko vyama vya siasa.

Balozi Dkt. Nchimbi alisema, uwepo wa Serikali hiyo Zanzibar umeondoa hali ya siasa za chuki na uhasama mkubwa uliokuwepo kabla ya kufikiwa kwa uamuzi wa kuundwa kwake, huku akisisitiza kuwa Chama Cha Mapinduzi kitaendelea kutimiza wajibu wake wa kutoa uongozi kwa nchi ili kudumisha umoja na utulivu uliokusudiwa kwa maslahi ya Wazanzibar na Watanzania wote.

Katibu Mkuu wa CCM Balozi Dkt. Nchimbi alisema hayo alipokuwa akizungumza na Wazee wa Zanzibar, Afisi Kuu ya CCM, Kisiwandui, Jumapili, Machi 24, 2024, ikiwa ni siku ya pili akiwa kwenye ziara ya kikazi, akitokea Pemba, ambako pia alifanya mazungumzo na mashauriano na Wazee wa Pemba, Jumamosi, Machi 23, 2024.

“Binafsi nikimsikia mtu anazungumzia kutaka kujitoa kwenye Serikali ya Umoja wa Kitaifa, simwelewi huyo mtu hata kidogo. Kwa sababu Serikali ya Umoja wa Kitaifa ilikuwa kwa ajili ya usalama wa maisha ya watu, usalama wa Wazanzibar, usalama wa Watanzania. Maisha ya watu ni muhimu sana kuliko kitu chochote. Tuliweka mbele maslahi ya nchi, utulivu na umoja wetu, si vyama vya siasa.

“Mnakumbuka wakati fulani nikiwa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, kila siku nenda rudi kwa helkopita kuja Zanzibar. Tulikuwa tunahangaika kuondosha uhasama na chuki. Najua kuna wakati wenzetu wanapata gadhabu na kuzungumza kwa jazba. Sisi wanaCCM tusiende huko hata kidogo. Sisi ndiyo Chama tawala. Sisi ni walezi. Mlezi hasusi. Tusiache wajibu wetu wa kulea hata kidogo. Mtoto ndiye anasusa. Na katika hili naombeni sana wazee wote wa Zanzibar na Tanzania, mniunge mkono,” alisema Balozi Dkt. Nchimbi.

Aidha, Katibu Mkuu wa CCM Balozi Dkt. Nchimbi pia alisisitiza msimamo wa CCM kuendeleza kutimiza wajibu wa kipekee wa kuyalinda Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar na misingi yake, akisema kuwa ndiyo yaliyowaweka watu wote kuwa sawa mbele ya sheria na kuondoa kila aina ya ubaguzi, ukiwemo wa matabaka, rangi na hali ya mtu.

“Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar yameondoa matabaka. Yakaleta utu, sote tunaunganishwa na utu wetu. Tunao wajibu wa kipekee kuhakikisha tunaendelea kulinda misingi ya Mapinduzi. Tuko tayari kuendelea kuyalinda. Hakuna umbo au rangi au hali inampatia haki zaidi mtu mwingine kuliko mwingine. Ukifanya ubaguzi wa namna hiyo wewe ni kaburu tun a ukaburu hauna rangi. Huo ndiyo msimamo wa CCM,” alisema Dkt. Nchimbi.

Akiwakaribisha katika mazungumzo hayo, Katibu Mkuu Balozi Dkt. Nchimbi aliwaambia Wazee wa Zanzibar kuwa wao ni mashahidi jinsi ambavyo awamu tofauti tofauti za Serikali za CCM, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, zimefanya kazi kubwa ya maendeleo ya watu na vitu, akiwakumbusha kuwa wasisite kuendelea kutoa ushauri au maelekezo ili kuhakikisha CCM inaendelea kuongoza kwa kuzingatia misingi ya kuundwa na kuanzishwa kwake, ikiwemo kuwatumia watu na kubadili hali yao ya maisha.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here