Rais Samia atoa maagizo kwa Wizara 5

0
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akizungumza na Viongozi pamoja na wananchi wa Mikoa ya Pwani na Morogoro kabla ya kuzindua Shughuli ya Kufunga Njia ya Kuchepusha Maji na Kuanza Ujazaji wa Maji kwenye Bwawa la Kuzalisha Umeme (Megawati 2115) la Julius Nyerere (JNHPP) kwenye Mto Rufiji Mkoani Pwani Desemba 22, 2022.

Na Beatrice Sanga, MAELEZO

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dokta Samia Suluhu Hassan ameziagiza Wizara 5 za Kisekta Nchini ikiwemo Kilimo, Uvuvi, Maji Mazingira pamoja na Ufugaji kuketi na kutumia nafasi zitokanazo na Bwawa la Kufua Umeme la Julius Nyerere.

Rais Samia alisisitiza uhifadhi wa mazingira katika vyanzo vya maji vinavyo jaza Mto Rufiji kutokana na umuhimu wa Mto huo katika Mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere.

Alitoa maagizo Rufiji Mkoani Pwani wakati wa ufunguzi ujazaji maji katika Bwawa la Mwalimu Nyerere ambapo alisema, kwa sasa Sekta zote zenye nafasi ya kuvutia wawekezaji na kutengeneza fursa kutokana na maji ya Bwawa la Mwalimu Nyerere kufanya hivyo ikiwemo Sekta ya Kilimo na Maji ambao ndio watanifaika kupitia Bwawa la Mwalimu Nyerere.

“Nazielekeza Wizara ya Kilimo, Wizara ya Ardhi na TAMISEMI na mamlaka nyingine mkapime maeneo hayo na muyaweke katika mashamba makubwa kwa ajili ya kufanya mnada wa wazi kwa wawekezaji wa uhakika katika kilimo, nawasihi pia mtenge maeneo maalum kwa ajili ya wakulima wadogowadogo hasa wa maeneo hayo yatakayokuwa na Miundombinu ya umwagiliaji maji,” alisema Rais Samia.

Aidha, Rais Dkt. Samia ameagiza Wizara ya Mazingira kuchukua hatua dhidi ya waharibifu wa mazingira katika vyanzo vya maji katika mito na maeneo muhimu ambayo yanatumika kama chanzo cha maji katika Bwawa la Mwalimu Nyerere

“Ndugu wananchi manufaa ya Bwawa hili katika nyanja zote yanawezekana tu kama tutatunza mazingira katika vyanzo vya mabonde ya Mito inayoleta maji mabwawani hapa nataka nisisitize umuhimu wa kutunza mazingira kwani huu mradi tumeujenga kwa gharama kubwa na kwa kujinyima vitu vingi muhimu”

“Itakuwa ni dhambi kubwa kama hautatimiza malengo yake kwa sababu ya uzembe na ubinafsi wetu kwahiyo kulinda mazingira na kulinda mradi huu Sasa ni suala la kufa na kupona,” alisema Rais Samia.

Kwa upande wake Waziri wa Nishati January Makamba pamoja na Mkurugenzi wa TANESCO Maharage Chande walisema, Serikali inaendelea na mipango ya muda ya mrefu ya kukabiliana na changanoto ya umeme ikiwemo kujenga mabwawa manne pamoja na kuanzisha miradi mingine kupitia Nishati jadilifu ili kukabiliana na changamoto ya umeme.

“Tupo katika kupanga mbele na ukiangalia Ile chati yetu sisi Leo hii tunajua mpaka 2040 mradi gani utaingia kwenye gridi, tumejipanga kwa muda mrefu na sio kwa muda mfupi, tunachoomba ni subira tatizo la kukatika umeme litaisha,”

“Sisi tunataka ndani ya miaka ijayo ibaki historia kwamba chini ya uongozi wako Mheshimiwa Rais ndipo ulimaliza shida yote ya umeme ya kudumu na Hilo ndilo tunalolifanya na subira tunayo na na mipango tunayo hivi Leo tunavyozungumza tuna mabwawa mengine mawili ambayo tunatafutia wakandarasi,” alisema Makamba.

Katika hafla hiyo pia imehudhuriwa na viongozi kutoka nchini Misri, Spika wa Bunge Tullia Akson, Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara Abdulahman Kinana ambapo wakizungumza katika hafla hiyo wameutaja Mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere kama moja ya Mradi utakao leta mapinduzi katika Sekta ya Nishati ambayo ni muhimu kwa maendeleo.

Hata hivyo, pamoja na zoezi la kubofya kitufe kuashiria kuanza kujaza maji, Rais Samia amepokea tuzo sanjari na Marais Wastaafu kutokana na kufanikisha ndoto za ujenzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere ambalo likikamilika litazalisha Megawati 2115

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here