RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ametunukiwa Tuzo Maalum ya kuwa Mhamasishaji Bora wa Sekta ya Uwekezaji Zanzibar.
Kwa kutambua mchango na juhudi zake za kufungua milango ya uwekezaji Zanzibar, ikiwemo kukifungua kiuchumi Kisiwa cha Pemba na kuwavutia wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi.
Tuzo hiyo imetolewa na Mamlaka ya Uwekezaji Zanzibar (ZIPA) katika hafla ya Chakula cha Usiku kilichoandaliwa na Mamlaka hiyo katika Hoteli ya Golden Tulip, Airport, Mkoa wa Mjini Magharibi jana Juni 17, 2025.
Akizungumza katika hafla hiyo, Rais Dkt. Mwinyi amewapongeza wadau mbalimbali kwa kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kukuza uwekezaji, hatua ambayo amesema inaelekea kufanikisha dhamira ya kuifanya Zanzibar kuwa kituo bora cha uwekezaji kitakachotambulika kimataifa.
Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amewapongeza wawekezaji wote waliotunukiwa tuzo mbalimbali katika hafla hiyo, akizielezea kuwa ni muhimu kwa kuthamini na kutambua mchango wao katika maendeleo ya nchi.
Rais Dkt. Mwinyi amewahakikishia wawekezaji kuwa kwa msingi wa mazingira tulivu ya kisiasa, kasi ya uimarishaji wa miundombinu, pamoja na sera bora, thabiti na rafiki kwa biashara, Zanzibar ipo katika nafasi madhubuti ya kuwa lango kuu la uwekezaji wa sasa na wa baadaye.
Hafla hiyo pia iliambatana na utoaji wa tuzo mbalimbali za ubora na umahiri kwa wawekezaji bora, ambapo Rais Dkt. Mwinyi aliwakabidhi tuzo hizo.