Mbeto: Jussa hana mbavu za kushindana na CCM Z’bar

0

Na Mwandishi Maalum, Zanzibar

CHAMA Cha Mapinduzi ( CCM) kimemtaka Makamu Mwenyekiti wa ACT Wazalendo, Ismail Jussa Ladhu, kushughulika na matatizo yaliyomo ndani ya chama chake kwakuwa CCM hana ubavu wa kushindana nacho.

Hayo yameelezwa na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar, Idara ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Khamis Mbeto Khamis, aliyemtaka Jussa akisubiri kimbunga kitakachokipeperusha ACT Oktoba mwaka huu.

Mbeto alisema, Jussa hajui yalioko Serikalini wala hafahamu takwimu na data za wanachama hai au wapiga kura ambao watakipatia ushindi CCM .

Alisema, anamtambua vizuri Jussa kama ni kasuku wa kisiasa ambaye sauti na uso wake hauna staha wala aibu, ndio maana huthubutu hata kubeza maendeleo yanayoonekana Zanzibar kwa wakati huu.

“Mwambieni Jussa apuunguze usanii na porojo kwenye majukwaa ya siasa ameschokwa na Wananchi. Siasa za kibaguzi dhidi ya wazanzibari zimegonga ukuta. Anaowataka waamini kama hakuna maendeleo wanamsikiliza, wakimcheka na kumpuuza,” alisema Mbeto.

Aidha, alimtaka Makamu Mwenyekiti huyo iwapo ana ushahidi wa kutosha dhidi ya SMZ ikihusika na ubadhirifu wa Mamilioni ya fedha za umma, ruksa afungue mashtaka mahakamani.

“Oktoba mwaka huu panapo uhai na uzima itafika. Mpira utawekwa katikati ya kiwanja. Mwamuzi atapuliza kipyenga. Mchezo utachezwa na wananchi wataamua ipi mbivu na mbichi,” alieleza Mbeto.

Pia, Katibu huyo Mwenezi, alisema hata kama Jussa ataendelea kulitumia jina la Hayati Maalim Seif Sharif Hamad, akidhani ACT kitapata mtaji wa kuungwa mkono, hakiwezi kushinda Oktoba.

Hata hivyo, Mbeto alimuasa Jussa na kumtaka aache siasa za ubaguzi, kwani Zanzibar kama kungekuwa na siasa za kubaguana kwa asili na nasaba, yeye ndiye aliyestahili kubaguliwa kuliko mtu yeyote.

“CCM , Zanzibar na Tanzania zimekataa siasa za ubaguzi wa aina yoyote. Tulipinga siasa aina ya siasa hizo kila mahali duniani. Jussa huna uwezo wa kumbagua yeyote Zanzibar kabla wewe hajabaguliwa” alieleza.

Mbeto alimueleza Jussa maamuzi ya CCM yatabaki kuwa ya CCM, kwani hata ACT Wazalendo kilianza kutangaza jina la Masoud Othman kama ndiye mgombea urais miaka mitatu iliyopita.

“Miaka mitatu iliopita Jussa na wenzake ndani ya ACT walimtangaza Othman atawania urais mwaka 2025 Zanzibar. Alipata wapi idhidi ya kutamka hivyo bila azimio la Mkutano Mkuu wa Taifa wa ACT? “alihoji Mbeto.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here