IDARA ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo CCM, Kamati maalum ya NEC Zanzibar imemshangaa Mwenyekiti wa ACT Wazalendo, Othman Masoud Othman kutojua itifaki za safari za viongozi na kujikuta akikwama kuingia katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Angola.
Pia, idara hiyo imesema endapo Othman hajui hata utaratibu wa safari za nje, kushindwa kuujulisha ubalozi ni wazi hana uwezo wa kuwa Rais wa Zanzibar.
Hayo yameelezwa na Mjumbe wa NEC na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar, Khamis Mbeto Khamis, ambapo alisema kiongozi huyo amelitia aibu Taifa.
Mbeto alisema, kutokana na wadhifa wake wa Makamo wa Kwanza wa Rais SMZ, alitakiwa kuaga kazini, kutoa taarifa Wizara ya Mambo ya Nje na kujulisha Ubalozi wa Tanzania Angola.
Aliongeza, taratibu hizo humfanya kiongozi wa Serikali kuanza kuandaliwa taratibu za kiitifaki , kiusalama na za kidiplomasia.
“Mwenyekiti wa ACT ametuabisha kwa kukiuka taratibu na itifaki za kidiplomasia. Makamo wa kwanza wa Rais hawezi kuingia nchi yoyote kienyeji, lazima taratibu zifuatwe na maafisa ubalozi wazisimamie,” alisema Mbeto.
Aidha, alisema hata kama Mwenyekiti wa ACT alikuwa na mpango wa kukutana na viongozi wa UNITA ili kujifunza sera, mbinu na mikakati ya kimapambano, alipaswa kufuata taratibu.
“Kabla ya kwenda Angola OMO alishatoa msimamo wa ACT wa kuweka kando siasa za maridhiano na kuanzisha mapambano. UNITA cha Angola na RENAMO cha Msumbiji, vina uzoefu mkubwa wa siasa za mapambano,” alieleza Mbeto.
Viongozi waliowahi kuviongoza UNITA cha Angala na Renamo cha Msumbiji ni Jonas Savimbi na Alfonso Dlakama ambao sasa wote ni marehemu.
Katika maelezo ya Katibu huyo Mwenezi, dunia nzima inajua Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, hivyo kiongozi kutoka upande wowote, hupokewa kwa uzito uleule.
”CCM itaendelea kuamini na kufanya siasa za kimaridhiano. Hakitajiingiza katika siasa za kimapambano. Wakati wa mapambano umepita. Afrika nzima sasa iko huru. Kutangaza za mapambano ni kutamani sera za kiharamia” alisema Mbeto.
Hata hivyo, alivitaka vyama vya upinzani vya Tanzania, kutambua kuwa mchango wa Tanzania katika nchi za Kusini mwa Afrika unaheshimiwa lakini pia CCM na vyama vya vilivyokuwa vua ukombozi ni ndugu wa damu.