Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
KATIBU wa Kamati Maalum ya NEC, Idara ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Khamis Mbeto Khamis amewaonya ACT Wazalendo kutokulichafua daftari la kudumu la wapiga kura kwa kuwazuia watu wa mkoa wa Mjini Magharibi ‘B’ kwenda kujiandikisha.
Akizungumza Mjini Unguja leo Mbeto alisema, kuna taarifa ya kuwepo makundi ya vijana wa ACT Wazalendo na viongozi wao wanaokaa njiani na kuwazuia watu wanaokwenda kujiandikisha kupiga kura.
Alisema, vyombo vya ulinzi na usalama vinapaswa kuwachukulia hatua viongozi hao wa ACT Wazalendo kwa kuwa wanachofanya kina lengo la kuvuruga amani na kuharibu mwenendo mzuri wa uandikishaji katika daftari la wapiga kura.
“CCM tunafuatilia kwa makini na tunatoa taarifa kwa umma ili kuviomba vyombo vya ulinzi na usalama kuchukua hatua kuhakikisha hao watu wanadhibitiwa na vitendo hivyo haviendelei tena Mkoa wa Mjini na Magharibi yote kwa ujumla,” alisema.
Mwenezi huyo amewaonya ACT Wazalendo kuacha kuwazuia watu njiani, kuwapa vitisho, kuwashawishi watu kutokwenda na kufanya fujo vituoni kwa kulazimisha wasio na sifa waandikishwe huku wakijua wazi kufanya hivyo ni kinyume na sheria ya tume ya uchaguzi Zanzibar namba nne ya mwaka 2018 Ibara ya 15 inayotaja sifa za watu wanaostahili kuandikishwa.
“Nahimiza wananchi kujitokeza kwa wingi kwenda kujiandikisha na kuviomba vyombo vya ulinzi na usalama kudhibiti hali hiyo ya ya makundi ya ACT Wazalendo kuwazuia watu kutumia haki yao ya kidemokrasia ya kujiandikisha ili wapate sifa ya kupiga kura” alisema Mbeto.
Mbeto alisema hayo kufuatia vurugu zilizofanywa na wafuasi wa ACT Wazalendo leo Machi 3 mwaka huu 2025, maeneo mbalimbali katika vituo vya Magharibi ‘B’ kuwashawishi watu wasijitokeze kujiandikisha.
Alisema, viongozi wa ACT Wazalendo wakiwa kwenye gari lenye namba za usajili Z 280 FQ aina ya Prado rangi ya Fedha (Silver), walikuwa wanapita kuwashawishi watu wasijiandikishe eneo la Magharibi ‘B’.
Katika tukio jingine, katika kituo cha afya Mbweni, mwanachama wa ACT Wazalendo, Sabah Khamis Abdallah amekuwa akifanya harakati za kuzuia watu wasijiandikishe kinyume na taratibu za Tume ya Uchaguzi Zanzibar.
Mbeto alibainisha kuwa, Waziri Mstaafu wa CUF ambaye ni mwanachama wa ACT, Abdilah Jihad Hassan alikuwa akizuia watu kwenda kujiandikisha katika kituo cha Viwanda Vidogo Vidogo.
Awali, Machi Mosi mwaka huu 2025 Katibu Mwenezi wa tawi la Magufuli, Abubakar Hussein Said alishambuliwa kwa kupigwa na fimbo na kujeruhiwa kichwani na mwanachama wa ACT Wazalendo.
Alisema, tukio hilo lilitokea eneo la CCM tawi la Uholanzi majira ya saa tano asubuhi baada kukataa kusimama aliposimamishwa na wafuasi wa ACT Wazalendo akiwa amembeba mama mjamzito aliyekuwa anampeleka kituo cha kujiandikisha.
“Katibu wa Jimbo la Welezo ACT Wazalendo Salum Kipara amekuwa akiwazuia watu kwenda kujiandikisha na alianza wakati uandikishwaji ukiwa Magharibi ‘A’ na sasa anafanya hivyo Magharibi ‘B’ alisema Mbeto.
Katika hatua nyingine Mbeto aliwashangaa ACT Wazalendo ambao kupitia mwanasheria wao wamedai kutaka kumshtaki Mkuu wa wilaya ya Kati, Sadifa Juma Khamis ya kuwakamata na kuwaweka ndani vijana wa ACT Wazalendo waliokusanyika ndani ya Mita 200 katika kituo cha kuandikisha wapiga kura na kubainisha kuwa sheria ya Tume ya Uchaguzi Zanzibar, inakataza walichofanya.
Mbeto alisema, Sheria namba 4 ya mwaka 2018 Ibara ya 15 ya Tume ya Uchaguzi Zanzibar mtu asiyehusika anatakiwa akae Mita 200 kutoka kituo kilipo na wanaotakiwa kuwepo eneo la kituo ni maofisa wasaidizi wa tume, Sheha wa Shia husika, mawakala wa vyama, polisi na waangalizi wenye vitambulisho maalum.