Tanzania yaahidiwa makubwa na Benki ya Dunia

0
Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia anayesimamia nchi za Kanda ya Mashariki na Kusini mwa Afrika, Victoria Kwakwa.

Na Benny Mwaipaja, Washington, DC

MAKAMU Rais wa Benki ya Dunia anayesimamia Kanda ya Mashariki na Kusini mwa Afrika, Victoria Kwakwa, ameahidi kuwa Benki yake itaendelea kuiunga mkono Tanzania katika kufanikisha malengo yake ya kukuza uchumi na kuwahudumia wananchi wake huku akipongeza hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali katika kusimamia uchumi wake.

Kwakwa ametoa pongezi hizo Jijini Washington D.C nchini Marekani, alipokutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa Tanzania, ukiongozwa na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Mwigulu Nchemba, kwenye mikutano ya kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF.

Alisema, uchumi wa Tanzania umekuwa tulivu na umekua kwa kasi ikilinganishwa na nchi nyingine anazozisimamia zilizoko Kanda ya Mashariki na Kusini mwa Afrika, ambazo zinahaha kujikwamua kiuchumi kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo msukosuko wa uchumi unaotokana na vita baina ya Urusi na Ukraine, pamoja na madhara ya UVIKO-19

Aliishauri Serikali kuendelea kusimamia kikamilifu sera nzuri za fedha na uchumi zinazoleta utulivu kwenye uchumi na kuhakikisha inaendelea kudhibii mfumuko wa bei pamoja na kuweka mipango endelevu ya kuishirikisha zaidi sekta binafsi katika shughuli za kiuchumi.

Kwakwa aliahidi kuwa, Benki yake itaendelea kuipatia fedha Tanzania kupitia madirisha mbalimbali ili iweze kutekeleza miradi mbalimbali inayoweza kuchochea ukuaji wa uchumi kwa haraka, ikiwemo sekta za nishati, kilimo, maji na ujenzi wa miundombinu wezeshi ya kukuza uchumi wa tai ana wananchi kwa ujumla.

Makamu huyo wa Rais wa Benki ya Dunia alisema, mfumuko wa bei ni kama kodi mbaya inayowaumiza zaidi wananchi masikini na kwamba Benki yake itaitumia Tanzania kama kielelezo na mfano wa kuigwa na nchi nyingine duniani.

Kwa upande wake, Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, aliishukuru Benki ya Dunia kwa pongezi hizo kwa usimamizi mzuri wa sera za uchumi na fedha na kuahidi kumfikishia pongezi hizo Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Aidha, Dkt. Nchemba alirejea kutoa shukrani zake kwa Benki hiyo kwa msaada mkubwa wa ushauri wa kitaalam na rasilimali fedha, unaotolewa na Benki hiyo kwa Tanzania na kuchangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya nchi na hivyo kupunguza umasikini wa watu wake.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango-Zanzibar, Dkt. Saada Salum Mkuya, alisema kuwa Benki ya Dunia ni mdau mkubwa wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kusaidia fedha na misaada inayotumika kuboresha sekta mbalimbali za kiuchumi na kijamii.

Alisema kuwa hivi sasa, Zanzibar, inafanya mageuzi makubwa ya kiuchumi kupitia sera ya uchumi wa buluu ikiwemo matumizi ya bahari na sekta ya utalii na kwamba Benki ya Dunia ni mdau mkubwa wa kufanikisha sera hiyo ambayo imelenga kuikwamua jamii ili iondokane na umasikini.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here