TANZANIA imefanya majadiliano na nchi ya Hungary ili kufanikisha utekelezaji wa mradi wa maji wa Biharamulo.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Mahomud Thabit Kombo ameongoza majadiliano hayo yaliyohusu mkopo wa masharti nafuu kutoka Serikali ya Hungary kwa lengo la kutekeleza Mradi wa Usambazaji Maji wa Biharamulo.
Majadiliano yamefanyika katika ofisi ndogo za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki jijini Dar es Salaam kati ya serikali ya Tanzania pamoja na ujumbe kutoka Hungary ukiongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Biashara wa nchi hiyo Peter Szijjarto.
Kombo amesema mradi huo ni sehemu ya jitihada za serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha jamii ya inaondokana na uhaba wa huduma ya majisafi na salama.
Amesema mradi huo unategemea kutumia teknolojia za kisasa za kusafirisha maji kutoka ziwa Victoria na kuyatibu kabla ya kufikisha kwa wananchi.
Naye Peter Szijjarto amesema serikali ya Tanzania imekuwa mshirika mzuri wa maendeleo na serikali ya Hungary. Amesema uhusiano huo ndio umewezesha kuleta mradi huo wa masharti nafuu kwa usalama wa afya ya wananchi na Afrika kwa ujumla.
Ziara ya Waziri Szijjarto pamoja na majadiliano kuhusu sekta ya maji inalenga kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia na kiuchumi baina ya Tanzania na Hungary