SERIKALI ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Japan zimetia saini Hati ya Makubaliano ya ushirikiano katika mpango wa pamoja wa uwekezaji katika Biashara ya Kaboni utakaowezesha kampuni za nchi hizo mbili kuwekeza katika Biashara ya Kaboni nchini Tanzania.
Utiaji saini wa makubaliano hayo umefanyika Mei 28, 2025 Tokyo, Japan kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ikiongozwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhandisi Hamad Yussuf Masauni na Serikali ya Japan ikiongozwa na Waziri wa Mazingira, Asao Keiichiro (Kei).
Akizungumza mara baada ya utiaji saini huo, Waziri Masauni amesema Makubaliano ya Mashirikiano yaliyosainiwa yamekusudiwa kuimarisha uhusiano kati ya Japan na Tanzania kwa maendeleo endelevu na hatua za kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi.
Alisema, ushirikiano huu utaongeza fursa ya kupanua soko la Biashara ya Kaboni kutoka kwa wawekezaji wa Japan watakaowekeza katika miradi ya biashara ya Kaboni itakayoibuliwa nchini.
Waziri Masauni alieleza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan anawataka wataalamu kutoka nchi hizi mbili kufanya kazi haraka, kwa bidii na kwa pamoja kwa manufaa ya nchi zote mbili ili kuhakikisha kuwa makubaliano hayo yanakwenda katika hatua ya utekelezaji.
“Tuko tayari kufanya kazi kwa ukaribu na wenzetu wa Japan ili kuhakikisha makubaliano haya yanatekelezwa kwa faida ya nchi zote mbili. Tayari Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeimarisha uwezo wa kitaasisi na kisheria katika usimamizi wa Biashara ya Kaboni ambapo Ofisi ya Makamu wa Rais iliandaa kanuni za mwaka 2022 za kuratibu biashara ya Kaboniā, alisisitiza Masauni.
Aidha, Mhandisi alibainisha kuwa katika Mfumo wa Kitaasisi, Serikali imeanzisha Kituo cha Taifa cha Ufuatiliaji wa Kaboni (NCMC) kupitia Sheria ya Usimamizi wa Mazingira iliyofanyiwa marekebisho ya 2025.
Hafla ya utiaji saini ilihudhuriwa na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Mhandisi Cyprian Luhemeja na Watendaji kutoka Ofisi hiyo.