JUKWAA la Kimataifa la “NewsBytes” limeitaja Hifadhi ya Taifa Serengeti kuwa kinara wa uhamasishaji wa utalii endelevu barani Afrika
Kupitia makala ya “ Five Wildlife Sanctuaries Promoting Sustainable Tourism” iliyochapishwa Juni 12, 2025 imeitaja Serengeti kuwa kinara katika juhudi zake za kulinda mazingira, kuhifadhi bioanuwai na kushirikisha jamii katika shughuli za uhifadhi na utalii kwa ajili ya maendeleo endelevu ya sekta ya utalii nchini.
Mbali na Serengeti, “NewsBytes” pia imezitaja hifadhi nyingine bora kwa utalii endelevu barani Afrika kama vile Kruger (Afrika Kusini), Maasai Mara (Kenya), Bwingi (Uganda) na Etosha (Namibia) ambapo hifadhi hizo zinajulikana kwa juhudi za uhifadhi, utalii endelevu na ushirikishwaji wa jamii.
Kutajwa kwa Hifadhi ya Taifa Serengeti ni ishara kuwa Tanzania inaendelea kuwa kinara katika uhifadhi wa kisasa unaojali mazingira na jamii.
Vivutio kama uhamaji wa Nyumbu (The Great Wildebeest Migration), wanyama wakubwa watano maarufu kama “The Big Five” na mandhari ya kuvutia vinaifanya Serengeti kuendelea kuzishinda hifadhi nyingi barani Afrika na dunia kwa ujumla.