Geita wapata kiwanda chenye viwango cha kusafisha dhahabu

0

Na Mwandishi Wetu

RAIS Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amezindua Kiwanda cha Kusafisha Dhahabu (Geita Gold Refinary – GGR) kilichopo Mkoani Geita, ambacho ni ndoto ya muda mrefu ya wananchi wa Mkoa huo.

Taarifa zinaonyesha kuwa, kwa mara ya kwanza mwekezaji anayemiliki kiwanda hicho Mama Sarah Masasi aliwasili Mkoani Geita Februari 25, 2019 na kueleza nia yake ya kutaka kuwekeza kwenye sekta ya madini hususani dhahabu.

Mwekezaji huyo ambaye ni raia wa Tanzania, alieleza nia yake ya kutaka kuweka mtambo wa uongezaji ubora Madini ya Dhahabu na wakati huo alipokewa na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Geita Injinia Robert Gabriel.

Baada ya kupokelewa na timu iliyosheheni wataalam kutoka katika mnyororo mzima wa kufanikisha uanzishwaji wa kiwanda wakiwemo wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira, TARURA na wengineo, Mama Masasi alisema, amefarijika kwa mapokezi hayo akiamini uwepo wa timu hiyo utachangia mafanikio makubwa kwake katika kuanzisha shughuli hiyo muhimu.

“Mimi ni Mtendaji na mtekelezaji, nisingependa kusema maneno mengi kwa kuwa nimekuwa nikishughulikia jambo hili tangu miaka minne iliyopita, baada ya Serikali kuhamasisha ujenzi wa viwanda hivi, hatimaye leo nimefika, nashukuru sana RC na watu wako. Ningependa kuhakikishiwa kupata eneo la ukubwa wa heka 4.5 likiwa mahali salama, lakini vile vile malighafi isiyopungua tani hamsini hadi themanini kwa mwaka,” alisema Mama Masasi.

Mama Masasi aliendelea kusema kuwa, mitambo itakayotumika itawekwa na Kampuni ya Kimataifa ya Bactrac Company Technologies (TERA) inayoaminika duniani ambayo pia ina uwezo wa kutenganisha madini ya dhahabu na madini ambatana, hivyo akasema angependa kuhakikishiwa uwepo wa mazingira mazuri kiuwekezaji baina ya pande zote yani Serikali, Mwekezaji na Wateja wa Dhahabu.

Mama Masasi alimaliza kwa kusema, “ninasema kwa nia moja, asante Mungu kunifikisha hapa na kufahamiana na nanyi, ninaahidi kuwa mtumishi wenu nikihakikisha Geita inafahamika Kimataifa kwa uzalishaji Dhahabu na mjue ninawahitaji kila siku ya maisha ya mradi huu,”

Kwa upande wake Injinia Robert Gabriel alimweleza mwekezaji huyo kuwa, hakukosea kuja Geita na kisha kumhakikishia upatikanaji wa eneo la ukubwa wa heka 5 bure tofauti na maombi yake ya heka 4.5, pamoja na kumhakikishia usalama na upatikanaji wa malighafi dhahabu.

Aidha, alimhakikishia uwepo wa miundombinu yote itakayotosheleza uanzishwaji wa kiwanda hicho kisha kuambatana na ugeni wake kuelekea eneo litakapofunguliwa soko la dhahabu Mjini Geita na baadaye kwenye eneo la uwekezaji litakalojengwa kituo cha uwekezaji mkoani hapa.

Naye Charles Itembe ambaye ni Mkurugenzi Mkuu Azania Bank alisema, wao kama mkopeshaji wa mwekezaji huyo wangefurahi kuona anapata uhakika wa malighafi ili aweze kurudisha mkopo kutoka benki yao na kwamba, anaamini kutakuwa na akiba ya kutosha ya dhahabu.

Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Geita Dkt. Japhet Simeo kwa upande wake akawashauri watalaamu wa madini kuwa, ni vyema kuwa na taarifa kamili na sahihi ili kuepuka kumvunja moyo mwekezaji na kwamba taarifa atakazozipata zitamwezesha kuamua ni aina gani ya uwekezaji anaweza kuufanya.

Kwa upande wake Afisa Madini Mkazi Mkoa wa Geita Daniel Mapunda akamtoa hofu, lakini akaomba muda ili kuja na takwimu sahihi zitakazoweza kumhakikishia na kumpa ujasiri mwekezaji huyo kuhusu upatikanaji malighafi, huku akimwelekeza taratibu za kufuata akimsisitiza kuzingatia kipengele cha mahusiano kwa jamii itakayomzunguka, lakini vilevile ajira kwa wazawa.

Hivyo basi, kwa mara nyingine Agosti 29, 2019, Mama Sarah aliwasili Geita na kupokelewa kisha kupelekwa kwenye eneo atakalojenga mtambo wa Uongezaji Ubora Madini ya Dhahabu ambapo kama ilivyo sera ya mkoa huu wa kutokuwa na urasimu, Mama Sarah alipewa Kiwanja chenye ukubwa wa Ekari nane bure kilichopo Mtaa wa Bombambili, Kata ya Bombambili, pamoja na hati kutoka ofisi ya Mkurugenzi wa Mji geita japokuwa awali alitaka ekari tano.

Haikuishia hapo, bali ofisi hiyo ya Mkurugenzi wa Mji Geita ilianza kuchonga barabara yenye urefu wa KM. 3.5 kufikia eneo la mwekezaji huyo, ambapo TANESCO na Mamlaka ya Maji ya GEUWASA nao wakaanza taratibu za kufikisha miundombinu hiyo.

Mara baada ya hatua hizo kukamilika, mwekezaji akaanza ujenzi na ukakamilika, na hatimaye kiwanda hicho kimezinduliwa rasmi Oktoba 15, 2022, ambapo inaelezwa ni moja ya viwanda bora na chenye viwango vya hali ya juu na kitakachowasaidia wachimbaji wa madini wa mkoa huo na maeneo ya jirani kuongeza thamani ya madini yao.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here