MGOMBEA wa kiti cha Rais wa Zanzibar kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewataka Wazanzibari kuendelea kukiunga mkono Chama hicho akibainisha kuwa ndicho mhimili wa amani ya Tanzania ikiwemo Zanzibar.
Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, Septemba 17, 2025, katika mkutano wa kampeni uliofanyika Uwanja wa Kajengwa, Makunduchi, Mkoa wa Kusini Unguja, ambao umeongozwa na Mgombea wa kiti cha Urais kupitia wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia CCM, ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Akihutubia maelfu ya wananchi waliojitokeza, Dkt. Mwinyi amesema, Wazanzibari wana kila sababu ya kuichagua CCM ili iendelee kuleta maendeleo makubwa katika sekta mbalimbali za kijamii na kiuchumi.
Aidha, aliwaomba wananchi kujitokeza kwa wingi siku ya kupiga kura na kuhakikisha CCM inapata ushindi wa kishindo.
Kwa mujibu wa ratiba, kampeni za CCM zitaendelea kesho Septemba 18, 2025 kwa mkutano mkubwa utakaofanyika Nungwi, Mkoa wa Kaskazini Unguja.