Madeni mapya ya watumishi kudhibitiwa

0

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Mohamed Mchengerwa amesema Serikali imeendelea kudhibiti uzalishaji wa madeni mapya ya kimshahara na yasiyo ya kimshahara.

Mchengewa ameyasema hayo wakati wa kujibu hoja kuhusu Serikali kulipa kwa wakati madeni mbalimbali ya watumishi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa nchini ili kuondoa malimbikizo ya madeni.

Alisema, Serikali imeendelea kulipa madeni ya watumishi wa mamlaka za serikali za mitaa na katika mwaka 2023/24 Shilingi Bilioni 116.08 zimetolewa kwa ajili ya kulipa madeni ya watumishi ambapo, mishahara ni Shilingi Bilioni 32.22 na madeni yasiyo ya mishahara ni Shilingi Bilioni 83.85.

Alifafanua kuwa, katika mwaka 2024/25 hadi machi, 2025 madeni yenye thamani ya Shilingi Bilioni 78.75 yamelipwa, kati yake Shilingi Bilioni 16.32 ni madeni ya mshahara na Shilingi Bilioni 62.43 ni madeni yasiyo ya mshahara yanayojumuisha fedha za uhamisho, likizo na stahiki za watumishi.

Mchengerwa alisema, katika kuendelea kuhakikisha madeni yanaendelea kulipwa, Ofisi ya Rais-TAMISEMI kupitia Ofisi za Wakuu wa Mikoa imekamilisha zoezi la uhakiki wa madeni ya watumishi yasiyo ya mishahara kufikia juni 2024 ambapo Halmashauri 36 zimeonekana zinaweza kulipa zenyewe kutokana na mapato yao ya ndani na 145 hazina uwezo.

“Taarifa ya uhakiki imewasilishwa Wizara ya Fedha kwa ajili ya kuendelea na hatua zinazofuata.” alisema Mchengerwa.

Aidha, Mchengerwa alisema Serikali imedhibiti uzalishaji wa madeni mapya ya kimshahara kwa kuingiza kwa wakati watumishi wote wanaoajiriwa kwa mara ya kwanza katika ‘payroll’ ya Serikali, kuhakikisha marekebisho ya mishahara yanafanyika kabla ya mtumishi kupata barua ya kupanda daraja na kuingizwa kwenye ‘payroll’ ya Serikali posho za watumishi wanaokaimu madaraka.

Pia, katika kudhibiti uzalishaji wa madeni yasiyo ya kimshahara Serikali imeyadhibitiwa kwa kutoa ruzuku kwa ajili ya gharama za likizo, uhamisho na stahiki za viongozi.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here