WAZIRI wa Madini Anthony Mavunde amefanya mazungumzo na Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Marvel Gold, Timothy Strong juu ya uwekezaji wa kampuni hiyo kwenye sekta ya madini.
Kampuni hiyo kutoka nchini Australia imefika kujitambulisha na kuelezea mpango wao wa kuanzisha mgodi mkubwa wa dhahabu katika Wilaya ya Hanang’ Mkoa wa Manyara.
“Tumeichagua Tanzania kwasababu ni nchi ambayo ina amani na usalama na mazingira mazuri ya uwekezaji,na tumevutiwa na mpango mzuri wa Rais Dkt. Samia Hassan kuvutia uwekezaji nchini Tanzania,” alisema Strong.
Aliongeza, kampuni hiyo itafanya utafiti wa kina kwa kurusha ndege na baadaye kukamilisha hatua zote za utafiti wa madini.
Alieleza kuwa, kampuni hiyo inategemea kuanza zoezi la utafiti wa kina ifikapo Septemba, 2025.
Awali, akizungumza katika kikao hicho, Waziri Mavunde amewapongeza wadau hao kwa kuichagua Tanzania kufanya uwekezaji wao na kuwahakikishia kwamba Serikali itatoa ushirikiano wa kutosha kuhakikisha miradi kama hiyo yenye dhamira ya kukuza sekta ya madini inafanikiwa.
“Ninapokea watu wengi sana wenye nia kama ya kwenu, asilimia kubwa si wakweli kutekeleza mipango yao na wamekuwa na maneno mengi kuliko vitendo,” alisema Waziri Mavunde.
Aliongeza, ana amini kwamba Kampuni hiyo itafanya kazi kubwa ya utafiti ili kama nchi ifanikiwe kupata mradi mwingine mkubwa wa uchimbaji madini ya dhahabu Mkoani Manyara.