JMKF yawaongezea wasichana uwezo wa kujiamini na kutambua afya ya akili

0

Habari na Picha na JMKF


MAFUNZO ya siku moja ya “WASICHANA WASHIKA HATAMU” kwa vijana wa kike  40 yaliyoandaliwa na Taasisi za Jakaya Mrisho Kikwete Foundation (JMKF) kwa kushirikiana na Plan International Tanzania yameendeshwa na kuhitimishwa kwa mafanikio makubwa.

Mafunzo hayo yaliyofanyika katika hoteli ya Regency Park jijini Dar es Salaam, yalilenga kuwaongeza uwezo vijana na wasichana wa kujiamini, kutambua afya ya akili, kukuza ustawi wao hususan katika masuala ya lishe na ukakamavu, haki za mtoto wa kike pamoja na ufahamu wa sheria za nchi juu ya maswala hayo,  ni sehemu ya shughuli za kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Mtoto wa Kike duniani mwaka huu.

Kauli mbiu ya maadhimisho hayo Kitaifa inaenda sambamba na ile ya Siku ya Mtoto wa Kike Duniani  ya: “Wakati wetu ni sasa—haki zetu, mustakabali wetu”

Afisa Mtendaji Mkuu wa JMKF Vanessa Anyoti ameeleza  kwamba Siku ya Kimataifa ya Mtoto wa Kike imekuwa jukwaa muhimu katika kutambua haki za msichana pamoja na changamoto kubwa anazopambana nazo duniani, na kwamba sasa kuna wito wa kuchukuliwa kwa hatua za makusudi za kuleta mageuzi  kijamii na kisiasa ili kuondoa vizuizi mbalimbali vya ubaguzi na chuki vinavyoendelea kurudisha nyuma maendeleo ya wasichana.

“Tanzania inaungana na nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa katika kukuza ufahamu wa jamii juu ya masuala yanayowakabili wasichana na kuwapatia fursa ya kupaza sauti zao.

“Duniani, wasichana wanaendelea kukabiliana na changamoto za uongozi, elimu, masuala ya afya ya akili na ukatili wa kijinsia, wakati wao ndio mawakala wakuu wa mabadiliko katika jamii zao”, aliongeza. Anyoti.

Siku ya Kimataifa ya Mtoto wa Kike ni maadhimisho ya kila mwaka yanayotambulika kimataifa na kuadhimishwa mnamo Oktoba 11  ili kuwawezesha wasichana na kukuza sauti zao. 

Kama lilivyo toleo lake la watu wazima, yaani Siku ya Kimataifa ya Wanawake, iliyoadhimishwa Machi 8, Siku ya Kimataifa ya Mtoto wa Kike inatambua umuhimu, nguvu, na uwezo wa wasichana wa balehe kwa kuhimiza kufunguliwa kwa fursa zaidi kwao. 

Siku hii pia imetengwa kuondoa changamoto za kijinsia ambazo wasichana wadogo wanakabiliana nazo kote ulimwenguni, zikiwemo ndoa za utotoni, fursa duni za masomo, ukatili na ubaguzi.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here