Katibu wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar, Idara ya itikadi, Uenezi na Mafunzo, Khamis Mbeto Khamis
Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimesema Uongozi katika ngwe ya pili chini ya Rais Dkt. Hussein Ali Mwinyi utaiachia Zanzibar alama kwa Maendeleo ya Nchi na Watu wake ambazo zitabaki kuwa kumbukumbu zisizofutika.
Katibu wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar, Idara ya itikadi, Uenezi na Mafunzo, Khamis Mbeto Khamis ameeleza hayo mbele ya Waandishi wa Habari Ofisi kwake Kisiwandui Mjini Unguja.
Katika maelezo yake, Mbeto aliitaja Ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kisasa huko Pemba na Barabara ya lami ya njia Nne toka Chake Chake hadi Mkoani yenye Umbali wa Kilomita 45.3 Mkoa wa Kusini Pemba.
Kadhalika Mbeto alisema utafanyika Ujenzi wa Uwanja mkubwa wa Soka ambao utatumika katika Michuano ya AFCON, unaochukua Watazamaji zaidi ya 40 elfu huko Fumba Mkoa wa Mjini Magharibi.
Pia, akataja kuna Ujenzi wa Barabara toka Tunguu – Makunduchi hadi Kizimkazi Mkoa wa Kusini Unguja wenye Umabli wa kilomita 47.
“Sera za CCM chini ya SMZ katika uongozi wa Rais Dkt. Mwinyi utaacha alama za kudumu. Alama hizo zitabaki kuwa kumbukumbu muhimu kwa maendeleo ya Wazanzibari wote,” alisema Mbeto.
Aidha, akiitaja Miradi mingine alisema ni Ujenzi wa Bandari ya abiria huko Maruhubi kwa Mpigaduri na Ujenzi wa Nyumba za Makaazi ya Watu za Kisiasa za wakaazi 10,000 Unguja na Pemba.
“Kutakuwa na Usafiri wa mfumo wa Mabasi ya Kisasa ya Abiria na watalii katika Mji wa Unguja. Pia zitajengwa treni zitakazopita kwenye barabara za lami. Ujenzi wa Barabara ya lami inayounganisha Mkoa wa Mjini na Kaskazini Unguja toka Kinazini hadi Bububu,” alieleza Mwenezi huyo.
Akifafanua zaidi alisema, kuna Mradi wa Uzalishaji wa Umeme utakaomaliza kero hiyo kwa Zanzibar, hospitali ya kufundishia ya kisasa na Chuo Kikuu cha Afya kitakachojengwa Binguni Mkoa wa Kusini Unguja.
“Serikali chini ya Utawala wa Rais Dkt. Mwinyi utaacha alama zisizofutika Unguja na Pemba. Atakapoondoka madarakani atakumbukwa kwa kuitumikia nchi na watu wake,” alieleza Mbeto.