NAIBU Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile amesema ameridhishwa na maendeleo ya utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya inayoendelea mkoani Kigoma, akibainisha kuwa uwekezaji huo una lengo la kuufungua mkoa huo kiuchumi na kuimarisha usafirishaji katika Ukanda wa Maziwa Makuu.
Akizungumza Februari 19, 2026 baada ya kukagua miradi katika Bandari ya Kigoma na Kibirizi, Kihenzile amesema Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kuboresha miundombinu ya bandari ili kuongeza ufanisi wa huduma na mchango wa sekta ya uchukuzi katika uchumi wa Taifa.
Katika Bandari ya Kigoma, mradi unahusisha ujenzi wa gati la abiria, lenye urefu wa mita 130 na upana wa mita 50, barabara ya sakafu ngumu yenye urefu wa takribani mita 500 inayoingia na kutoka bandarini, pamoja na Jengo la abiria lenye uwezo wa kuhudumia abiria 200 hadi 250 kwa wakati mmoja.
Mradi huo unafadhiliwa kwa ruzuku (grant) kutoka Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japani (JICA) kwa thamani ya Dola za Marekani Milioni 16.9, na hadi sasa umefikia asilimia 9 ya utekelezaji wake ambapo kukamilika kwake kunatarajiwa kurahisisha usafirishaji wa abiria na mizigo, kuongeza ushindani wa bandari na kuimarisha biashara ya kikanda.
Mhe. Kihenzile pia amekagua mradi wa maboresho makubwa ya sehemu ya mizigo katika Bandari ya Kigoma, mradi ambao upo katika hatua za awali za makabidhiano ya eneo la utekelezaji ukilenga kuongeza uwezo wa kuhudumia mizigo, kuimarisha mapato ya Serikali kupitia tozo na kodi, pamoja na kufungua fursa za ajira kwa wananchi wa Kigoma na maeneo jirani.
Utekelezaji wake utawezesha mwekezaji kupitisha madini kupitia Bandari ya Kigoma badala ya kutumia njia ya Lobito nchini Angola.
Pia katika kuimarisha maendeleo ya jamii inayozunguka bandari kama sehemu ya utekelezaji wa mpango wa Uwajibikaji kwa Jamii ( CSR), TPA inatekeleza mradi wa usanifu na ujenzi wa Soko la Kisasa la Kibirizi pamoja na Kituo kipya cha Polisi.
Mradi huo wa thamani ya Shilingi Bilioni 6.4 utatekelezwa kwa muda wa mwaka mmoja na sasa upo katika hatua za mwisho za usanifu na maandalizi ya awali ya ujenzi.
Soko hilo la kisasa litakuwa na vibanda 250 na uwezo wa kuhudumia wafanyabiashara zaidi ya 500 kwa wakati mmoja, likilenga kutoa mazingira bora, salama na yenye hadhi kwa shughuli za biashara.
Mapema akimkaribisha Naibu Waziri, kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Mkurugenzi wa huduma za Uhandisi Mha. Erick Madinda, ametoa shukrani za pekee kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuwekeza katika miundombinu ya bandari za Bahari na Maziwa, akisisitiza kuwa miradi hiyo ni sehemu ya mkakati mpana wa kuifanya Kigoma kuwa lango muhimu la biashara na usafirishaji katika Ukanda wa Maziwa Makuu.
Kwa ujumla, utekelezaji wa miradi hiyo unaonesha dhamira thabiti ya Serikali ya kuongeza ufanisi wa bandari, kukuza mapato ya Taifa na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa Kigoma na Tanzania kwa ujumla.